TBF inachukua fursa hii kuufahamisha umma kuwa mashindano ya kikapu ya FIBA Zone V U18 (Wanawake na Wanaume ) yanatarajiwa kuanza tarehe 17 hadi 22 June, 2018 hapa Dar Es Salaam, Tanzania.
Ni matarajio yetu kuwa mmoja kati viongozi wetu wakuu wa nchi ndie atakuwa mgeni rasmi wa mashindano haya na yatarushwa mubashara (live) siku zote za mashindano na vituo vyote vikubwa vya TV na Radio ambavyo tumeviomba.
Gharama za maandalizi ya timu zetu 2 za Taifa na gharama kuandaa mashindano haya ni kubwa, na tayari kuna wadau wameshajitokeza kutoa ahadi na wengine wameshasaidia.
Hadi sasa hivi TBF ina upungufu wa takribani Tshs 100M, kati ya hizo Tshs. 60M ni za kuandaa mashindano na Tshs. 40M ni za kuweka timu zetu 2 za wanawake na wanaume kambini na kununua vifaa vya michezo zikiwemo Jersey za kucheza na za mazoezi, truck suits, viatu, socks, mipira na madawa.
Pia tuna mahitaji mengi ili kufanikisha matengenezo ya uwanja wa ndani wa Taifa (indoor) ukiacha kuvuja paa na kukatika kwa umeme ambako kutadhibitiwa na msaada ulitolewa na Mkuu wa Mkoa wa DSM Mhe. Paul Makonda. Katika uwanja huu wa Taifa bado kunahitajika matengenezo ya mfumo wa taa na vifaa vya umeme, mabomba, vyoo na mfumo wa maji, mabenchi ya kukalia, mfumo wa kutoa na kuingiza hewa (ventilation), na rangi ya kupaka ndani na nje ili kuweka mazingira ya uwanja yawe ya kuvutia.
Uwanja huu wa ndani wa Taifa utatumika kwa mashindano haya ya U18 June na pia baadae utatumika kwa mashindano ya kutafuta Klabu Bingwa wa Kikapu FIBA Zone V yanayotarajiwa kufanyika mwezi Septemba, 2018 hapa hapa Dar Es Salaam.
Pia kuna gharama za usafiri, posho na malazi ya Kocha wa Kigeni ambaye anatoka Minneapolis, Marekani, Coach Matthew McCollister ambaye tunataraji atafika nchini walau majuma 2 kabla ya kuanza mashindano haya ili kuzinoa timu zetu 2 kwa kushirikiana na jopo la makocha Wazalendo wakiongozwa na Coach Bahati Mgunda.
Tunatarajia mashindano ya FIBA Zone V U18 yatakayofanyika mwezi ujao yatashirikisha timu za Taifa 24, za wanawake na wanaume, kutoka nchi 12 za Misri, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia, Eritrea, Djibouti, Sudan, Somalia, Sudani Kusini na wenyeji Tanzania. Bingwa wa mashindano haya atapata nafasi ya kushiriki mashindano ya kutafuta bingwa wa Afrika (Afrobasket 2018) baadae mwaka huu.
Tunatarajia tutakuwa na wageni takribani 400 kutoka nchi mbali mbali ikiwa ni pamoja na maofisa kutoka FIBA, waandishi na wadau kutoka nchi husika.
Hivyo basi natoa wito kwa wapenzi wote wa michezo nchini, Serikali, taasisi za umma na binafsi, wafanyabiashara, wanasiasa, wafanyakazi na wananchi wote kwa ujumla kujitokeza na kushirikiana na TBF kufanikisha maandalizi mashindano haya ili ikiwezekana vikombe vyote vibaki nchini na kuzipatia nagasi timu zetu za Tanzania kushiriki Mashindano makubwa ya Kikapu ya FIBA Afrika.
Kushiriki na kuandaa mashindano ya kimataifa ni sehemu ya jitihada zetu za kuendelea kuitangaza nchi yetu kupitia michezo ili sekta hii nayo ishiriki kikamilifu katika kuchangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Taifa letu.
Tumuunge mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kila mtu kuwajibika katika eneo lake, kujenga Tanzania ya viwanda ili kusaidia ukuaji wa uchumi na hatimaye kuifanya nchi yetu kuwa na uchumi wa kipato cha kati haraka zaidi ya ilivyotarajiwa.
Michezo ni moja ya viwanda vikubwa vinavyotengeneza ajira nyingi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kama tutafanya uwekezaji sahihi.
Mchezo wa kikapu ni mchezo pekee nchini unaopendwa na watu wengi wa rika na jinsia zote kwa usawa. Hivyo basi kusaidia mchezo huu utakuwa umefanya sehemu kubwa ya kusaidia jitihada za Serikali za kusaidia na kuendeleza vijana wetu na kuchangia katika maendeleo ya Taifa letu kwa ujumla.
Naomba kila mwenye uwezo achangie kwa kadri atakavyojaliwa kupitia taasisi yake au mtu binafsi pia anakaribishwa kuchangia.
Pamoja tunaweza.
We Are Basketball
Phares Magesa
Rais,
Shirikisho la mpira wa kikapu Tanzania (TBF)
www.tbf.or.tz
Mag...@hotmail.com
+255 713 618320 (WhatsApp)
22 May, 2018.
N.B:
FIBA ni Shirikishp la Mpira wa Kikapu Duniani,
FIBA Africa ni Shirikisho la Mpira wa Kikapu Afrika,
FIBA Zone V ni Shirikisho la Mpira wa Kikapu kanda ya tano,
U18 ni Mashindano ya vijana chini ya miaka 18.
Sent from my Huawei Mobile