Migodi inavyochafua mazingira

18 views
Skip to first unread message

Nicomedes Kajungu

unread,
Oct 17, 2013, 12:46:28 AM10/17/13
to Spam Moderators, numet-med...@googlegroups.com
Migodi inavyochafua mazingira

Sitta Tumma

 

“ZIPO baadhi ya kampuni za migodi ya madini nchini zinafanya kazi zake kwa kukiuka sheria za mazingira. Mafuta hayapaswi kumwagwa eneo lisilokuwa limeandaliwa kitaalamu.”

Hiyo ni kauli ya Ofisa Mwandamizi wa Mazingira kutoka Timu ya Uchunguzi ya Baraza la Mazingira Tanzania (NEMC), Dk. Yohana Mtoni.

Dk. Mtoni ametoa kauli hiyo alipokutana na waandishi wa habari.

Akitoa ripoti ya ukaguzi uliofanywa na NEMC katika migodi tisa iliyopo mikoa ya Kanda ya Ziwa, kuanzia Agosti 25, mwaka huu anasema imeonesha kuna uchafuzi mkubwa wa mazingira unaofanywa na baadhi ya kampuni za migodi ya madini.

Dk. Mtoni anasema kupitia ripoti hiyo wamebaini ukiukwaji wa sheria za mazingira.

Anasema baadhi ya migodi hiyo inajihusisha na umwagaji ovyo wa mafuta na kemikali pamoja na utunzaji mbovu wa dawa zenye kemikali.

Uchafuzi mwingine wa mazingira unaofanyika ni utupaji wa taka ngumu, kushindwa kudhibiti majitaka yasiyosafishwa, mitaro inayotiririsha maji ya kemikali kutoka kwenye mabwawa ya majitaka kutokujengwa kitaalamu ili kuzuia kemikali kuingia ardhini na umwagaji ovyo wa maji yenye kemikali bila kuzingatia usalama wa mazingira.

Kutokana na hali hiyo, NEMC imelazimika kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya migodi saba mikubwa, kwa kuitoza faini ya sh milioni 450 kutokana na kukiuka sheria za mazingira.

Dk. Mtoni anaitaja migodi iliyobainika na uchafuzi wa mazingira kinyume cha sheria za nchi ni North Mara-Nyamongo, GGM na Buzwagi.

Migodi mingine ni Bulyanhulu, El-Hillal, Tulawaka na mgodi wa Resolute.

Uongozi wa GGM umesema utafanya mazungumzo ya wazi baina yake na serikali na NEMC juu ya faini hiyo.

Sheria hizi zinakataza uchafuzi wa mazingira. Na zinaamuru mtu au kampuni kukamatwa na kuamliwa kulipa faini ya fedha ama kuhukumiwa kifungo jela.

Si hilo tu, Sera ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 1997 nayo inasema: Udumishaji, usalama na matumizi sawa ya rasilimali kwa mahitaji ya msingi ya sasa na ya vizazi vijavyo, bila kuharibu mazingira au kuhatarisha afya na usalama.

“Kuzuia na kudhibiti uharibifu wa ardhi, maji, mimea na hewa ambayo ndiyo husaidia mfumo wa uhai wetu, kuhifadhi na kuendeleza urithi wetu na ule unaotengenezwa na binadamu, ikiwa ni pamoja na maisha ya viumbe wa aina mbalimbali na vya pekee nchini Tanzania.”

Tangu mwaka 1997 serikali ilipotunga Sera hii ya Taifa ya Mazingira, hatua mbalimbali zimechukuliwa na serikali, mashirika, taasisi na asasi kuhusu udhibiti na utunzaji wa mazingira.

Ninapozungumzia uchafuzi wa mazingira katika maeneo yetu ya makazi na sehemu za kazini, namaanisha kwamba tunaweka rehani maisha yetu na ya vizaji vijavyo, iwapo kila mmoja wetu hataamua kutunza mazingira.

Katika kupambana na hali hii ovu, lazima serikali kupitia idara zake za kudhibiti uchafuzi wa mazingira kama vile NEMC, LVEMP pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), itumie vema sheria zake kuwaadhibu watu au kampuni yanayokiuka sheria za nchi.

Ubutu wa matumizi ya sheria za mazingira, ndicho chanzo ninachokiona mimi kinachochea hali hii ya uchafuzi wa mazingira, maeneo mbalimbali ya nchi yakiwamo maeneo ya migodini.

Hatua zilizochukuliwa na NEMC dhidi ya kampuni hizo za migodi zisiishie hapo.

Ofisa Mazingira kutoka NEMC, Paul Kalokola, anasisitiza: “Licha ya kampuni hizo saba za migodi ya madini kuamliwa kulipa fedha, lakini ipo migodi mitatu tumeipa muda wa miezi mitatu kuweka mfumo mzuri wa utunzaji wa mazingira, la sivyo hatua kali zaidi za kisheria tutazichukua.”

Anaitaja migodi hiyo kuwa ni GGM, Bulyanhulu na Buzwagi. Na kwamba migodi hiyo itakuwa chini ya uangalizi wa muda huo na ikishindwa kutekeleza maagizo ya NEMC lazima hatua za kisheria zaidi zichukuliwe pasipo kuogopa ukubwa wa kampuni.

“NEMC na serikali kwa ujumla hatukubali hali hii, lazima tuchukue hatua za kisheria kali sana kwa wachafuzi wa mazingira,” anasisitiza Kalokola.

Ili Tanzania iweze kushinda vita hii ya uchafuzi wa mazingira lazima uwepo usimamizi na utekelezwaji thabiti wa mikataba mbalimbali ya kimataifa.

Katika mikataba hiyo, serikali yetu imeweka saini mikataba kadhaa ya mazingira na kuridhia makubaliano na nchi mbalimbali.

Kuna mapatano kwa ajili ya hifadhi, usimamizi na maendeleo ya mazingira ya bahari na mwambao wa Afrika Mashariki, pamoja na itifaki zinazohusika na mapatano hayo yaliyofikiwa Machi mosi 1996.

Mkataba wa Umoja wa Mataifa unaohusu mfumo wa mabadiliko ya hali ya hewa ulisainiwa Aprili, 1996.

Makubaliano ya Vienna ya kuhifadhi tabaka la ozoni na makubaliano ya Montreal juu ya vitu vinavyoharibu tabaka la ozoni yaliyosainiwa Aprili 7, 1993 na Aprili 16, 1993.

Mingine ni Mkataba wa Basley wa kudhibiti kusafirisha nje ya mipaka dawa zenye hatari na jinsi ya kuyateketeza uliowekwa saini Aprili 7, mwaka 1993; pamoja na makubaliano ya Bamako juu ya kuzuia kuingiza Afrika na kudhibiti kusafirisha nje ya mipaka dawa zenye hatari katika Afrika yaliyofikiwa Aprili 7, 1995.

Kwa mikataba hii ya kimataifa iliyoridhiwa na serikali iwapo watawala watatekeleza vema wajibu wao, ikiwa ni pamoja na kuzichukulia hatua kali za kisheria kampuni, taasisi, asasi, mashirika na watu binafsi wanaochafua mazingira, hakika Tanzania itang’ara ulimwenguni kwa kudhibiti uchafuzi huo wa mazingira.



0784 785294 sitta...@yahoo.com
_________________________________________________
Nicomedes M. Kajungu
General Secretary
National Union of  Mines and Energy Workers  of Tanzania.
(NUMET)
P.O.Box 7733, Mwanza.
 +255 782 315 688,  +255 767 48 32 71,      +255 719 451 850
Skype add: nkajungu
Reply all
Reply to author
Forward
Message has been deleted
Message has been deleted
0 new messages